UNFPA Yatoa Msaada wa Uzazi wa Mpango kwa Serikali ya Tanzania
Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu Duniani (UNFPA) limekabidhi tembe za uzazi wa mpango kwa Serikali ya Tanzania.
Akizungumza katika hafla fupi iliyofanyika Bohari ya Dawa (MSD), Mwakilishi wa UNFPA nchini Tanzania, Bw.Mark Bryan Schreiner, alisema msaada huo ni sehemu ya juhudi za UNFPA katika kuisaidia Serikali ya Tanzania kuboresha huduma za uzazi wa mpango kwa wananchi.
Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa mshirika mkubwa wa UNFPA, katika utekelezaji na uboreshaji wa huduma za uzazi wa mpango, jambo ambalo ni muhimu katika kuboresha afya za wananchi hasa maskini.
Naye mwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Dk Felix Bundala, aliishukuru UNFPA kwa kuendeleza ushirikiano mzuri kati yake na Tanzania hasa katika kuisaidia Tanzania katika masuala mbalimbali ya kuboresha huduma za afya.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai alisema MSD imepokea vidonge hivyo na jukumu la MSD ni kuhakikisha wanafika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini, lengo likiwa ni kuboresha huduma za afya hasa kwa mama na mtoto.