Kanda ya Mtwara
Kanda ya Mtwara ya Bohari ya Dawa ilianzishwa mwaka 1994, ikiwa ni lango muhimu la ugavi na usambazaji wa dawa na vifaa tiba eneo la Kusini mwa Tanzania. Kanda hii imewekwa kimkakati kuhudumia mikoa ya Mtwara na Lindi pamoja na Wilaya ya Tunduru-Mkoa wa Ruvuma. Kanda ya Mtwara ina jukumu kubwa la kuhakikisha dawa na vifaa tiba vinawafikia wananchi wote wa kusini mwa Tanzania.
Mawanda ya Utoaji Huduma
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, Kanda ya MSD Mtwara inahudumia jumla ya watu 3,241,029. Idadi hii inajumuisha
Mkoa wa Mtwara – watu 1,634,947,
Mkoa wa Lindi – watu 1,194,028, na
Wilaya ya Tunduru- Mkoa wa Ruvuma – watu 412,054
Kanda ya MSD Mtwara inahudumia jumla ya vituo vya kutolea huduma za afya 842, ikijumuisha vituo kuanzia ngazi ya msingi, ngazi ya kati, hadi ngazi ya taifa.
1. Vituo ngazi ya kati na taifa – Hospitali 1 ya Rufaa ya Kanda, na hospitali 2 za Rufaa za Mikoa.
2. Vituo ngazi ya msingi – Hospitali 15 za wilaya zilizo chini ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa – (TAMISEMI), hospitali teule 2 za Wilaya, vituo vya afya 57, zahanati 569,
3. Vituo vya Tasisi za kidini na taasisi nyingine za umma - Taasisi za dini 21, na taasisi nyingine za umma 50.
Uwezo wa Uhifadhi na Uendeshaji
Ili kuhudumia vituo vya afya ipasavyo na kwa ufanisi, kanda hii ina ghala lenye ukubwa wa eneo la mita za mraba 5,758 na magari 17 ya usambazaji yenye ukubwa tofauti kulingana na mahitaji. Rasilimali hizi kwa pamoja huiwezesha Kanda kutunza, na kusambaza dawa na vifaa tiba kwa ufanisi na kwa kuzingatia viwango vya juu vya ubora na usalama.
Mafanikio ya kanda ya MSD Mtwara yanatokana na uwapo wa timu ya wataalamu 41 ikihusisha wabobezi wa masuala ya ugavi ,wafamasia, wahasibu, wawakilishi wa mauzo, maofisa huduma kwa wateja, mafundi sanifu vifaa tiba na madereva. Mchango wao wa kitaalamu unahakikisha kuwa kanda hii inaendelea kuimarisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba, hivyo kuboresha utoaji wa huduma za afya na kuongeza ufanisi wa usambazaji katika maeneo yake.
Utoaji wa Huduma Bora
Kwa kuzingatia eneo lake la kimkakati, miundombinu ya kisasa, na nguvu kazi yenye ujuzi, Kanda ya MSD Mtwara inaendelea kuwa mhimili muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma za afya katika maeneo ya kusini mwa Tanzania.
Kanda hii pia, inaendelea kujidhatiti kutekeleza dira kuu ya MSD ya kuwa "Kituo Bora cha Umahiri katika Mnyororo wa Ugavi wa Bidhaa za Afya Barani Afrika".