MSD Yapongezwa kwa Maboresho ya Huduma, Ndani ya Muda Mfupi.
Naye Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Makorora mkoani Tanga, Dk Angelina Meshack ameipongeza serikali kupitia MSD baada ya kupokea vifaa vya chumba cha upasuaji kikiwemo kitanda cha upasuaji, mashine ya kulala na taa zinazotumika wakati wa upasuaji na kusema kuwa vifaa hivyo ni msaada mkubwa kwa kituo hicho kwani awali kulikuwa na changamoto katika utoaji wa huduma.
“Awali tulikuwa hatufanyi kabisa upasuaji hivyo tulipopokea fedha za ukarabati wa vyumba vya upasuaji tulifanya hivyo na baadaye vifaa hivyo vililetwa na MSD na kuanza kutoa huduma za upasuaji”. Alisema Dk Angelina
Alisema baada ya kupokea vifaa hivyo walianza kutoa huduma mbalimbali za upasuaji kwa wajawazito ikiwemo upasuaji mdogo kwani awali walikuwa wakipeleka wagonjwa katika Hospitali ya Bombo kwa kuwa huduma hiyo ilikuwa haipatikani kituoni hapo.
“Kwa ujio wa vifaa hivi, kumerahisisha mama mjamzito kutoa huduma za upasuaji moja kwa moja na tunaokoa maisha ya mama na mtoto”. Alisema.
Aidha, Dk Angelina alisema pia walipewa jenereta kwa ajili ya hospitali hiyo lakini waliamua kuwasiliana na ofisi ya mganga mkuu ili waweze kuichukua na kuikabidhi kwa vituo vingine ambavyo havina jenereta kwa sababu kituo hicho kilikuwa na jenereta ambayo walikuwa wameinunua awali.
Alieleza kuwa upatikanaji wa dawa katika kituo hicho ni mzuri kwani kwa sasa asilimia 90 ya dawa muhimu zipo na wanaendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.