MSD Yaadhimisha Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 kwa Kutoa Elimu ya Rasilimali Watu na Kunadi Bidhaa za Afya
Dodoma, Juni 17, 2026
Bohari ya Dawa (MSD) imeungana na taasisi nyingine za umma kuadhimisha Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 kwa kutoa elimu ya masuala ya rasilimali watu kwa watumishi wake na kuendelea kunadi bidhaa na huduma mbalimbali za afya kwa wananchi na wadau wanaotembelea maonesho hayo.
Katika kipindi chote cha maadhimisho hayo, watumishi wa MSD watapata fursa ya kushiriki kliniki maalumu ya rasilimali watu inayolenga kutoa elimu, ushauri na ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali ya kiutumishi. Miongoni mwa maeneo yatakayogusiwa ni haki na wajibu wa mtumishi, likizo, mifumo ya utumishi, mafao, kanuni za utumishi wa umma pamoja na huduma nyingine zinazotolewa na Idara ya Rasilimali Watu.
Pia, wananchi na wadau wanaotembelea banda la MSD katika viwanja vya maonesho watapata nafasi ya kujifunza kwa undani kuhusu majukumu ya taasisi hiyo, huduma zake za usimamizi wa ugavi wa bidhaa za afya nchini, pamoja na kufahamu aina mbalimbali za bidhaa za afya zinazohifadhiwa na kusambazwa na MSD kwa ajili ya kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 yanafanyika kuanzia Juni 16 hadi 23, 2026 katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma. Maadhimisho hayo yamefunguliwa rasmi leo tarehe 17 Juni, 2023 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete.
Kwa mwaka huu, maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Kuchochea Uwajibikaji kwa Huduma Endelevu,” ambayo inalenga kuhimiza taasisi za umma kuongeza uwajibikaji kwenye utoaji wa huduma bora na endelevu kwa wananchi.